Chama cha Kitaifa cha Walimu, KNUT kimepinga vikali pendekezo la Serikali Kuu kutumia shule za upili za mabweni kuwa maeneo ya kuwaweka karantini waathiriwa wa virusi vya korona.
Kupitia taarifa kwa vyombo vya habari, Katibu Mkuu wa KNUT Wilson Sossion ameitaka serikali kutafuta mbinu mbadala ya kuwaweka watu karantini , badala ya kutumia taasisi za elimu ili kuzuia unyanyapaa baada ya maambukizi kudhibitiwa.
Sossion aidha amepinga vikali shinikizo la kuahirishwa kwa mitihani ya kitaifa mwaka huu jinsi inavyopendekeza Chama cha Walimu wa Shule za Upili na Vyuo vya Kadri Kuppet. Kuppet kupitia Katibu wake Mkuu Akello Misiri, ameitaka serikali kuahirisha mitahani hiyo kutokana na kuzuka kwa virusi vya korona na kutatizwa kwa kalenda ya elimu nchini.
Sossioni vilevile, amependekeza kuwa walimu na wafanyakazi wote wa serikali kuondolewa kodi ya nyumba kwa kipindi cha miezi mitatu wakati huu mgumu wa maambukizi ya virusi vya korona.
Taarifa ya KNUT, imejiri siku moja tu baada ya KUPPET kuiomba serikali kuanzisha mpango wa kusambaza chakula kwa Wakenya kote na mgao fulani kwa kila mmoja ili kuwakwamua kiuchumi wakati huu mgumu.
Wizara ya Afya kwa ushirikiano na Serikali za Kuanti, inalenga kuzitenga shule 20 za upili za mabweni kuisaidia kuwaweka waathiriwa wa korona karantini. Pendekezo hilo vilevile, limepokea pingamizi kutoka kwa Kuppet inayosema kuwa serikali itumie maeneo wazi ya shule hizo wala si mabweni.