Waziri wa usalama wa ndani Fred matiangi na inspekta mkuu wa Polisi Hillary Mutyambai leo wamefika mbele ya kamati ya senate kuhusu usalama kufuatia kukamatwa kwa maseneta watatu siku ya jumatatu .
Spika wa senate Ken Lusaka alikariri msimamo wao aliposema kwamba wataungana wote kushinikiza kuachiliwa kwa viongozi hao na kuheshimiwa kwa bunge la senate .
Maseneta Steve Lelegwe (Samburu), Christopher Langat (Bomet) na Cleophas Malala (Kakamega) walikamatwa siku ya jumatatu kabla ya senate kujadili mswada tata wa ugavi wa mapato kwa kaunti .
Kufuatia kukamatwa kwao ,maseneta walibadilisha mjadala wao kutoka hoja hiyo na kuanza kutaka waachiliwe huru .
Lusaka aliishauri kamati ya usalama ya senate kuwaagiza wakuu wa vyombo vya usalama kufika mbele ya wanakamati hao na kueleza kilichotokea . Mwenyekiti wa kamati hiyo Yusuf Haji aliwaeleza maseneta baadaye kwamba walitumiwa ujumbe ulioeleza kuwa waziri Matiangi alikuwa likizo ya siku 10 ambayo mawaziri wote walipewa na rais Uhuru Kenyatta .